MMOJA
wa wajumbe wa Zanzibar wa lililokuwa Bunge Maalumu la Katiba amembana na
kumshika uwongo Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta, akisema yeye hakupiga
kura lakini mwenyekiti huyo na wenzake walichomeka jina lake ili kulazimisha
upatikanaji wa theluthi mbili ya Wazanzibari.
Mjumbe
huyo ambaye ni Makamu Mwenyekiti Taifa wa Chama cha NCCR-Mageuzi, Haji Ambar
Khamis, amesema kuwa ameshangaa kukuta jina lake kwenye orodha ya majina ya
wajumbe waliopiga kura kupitisha katiba inayopendekezwa. Jina la Khamis ni
nambari 39 katika ukurasa wa 209.
Akizungumza
na waandishi wa habari jana katika makao makuu ya chama, Ilala, Dar es Salaam,
huku akitokwa na machozi, Khamis alisema amesikitishwa na tukio hilo, na mpaka
sasa hana amani, na anahofia maisha yake.
“Mimi
sijashiriki kabisa bunge hilo tangu Aprili, na wala sijapiga kura. Sijui nini
kinaendelea mpaka jina langu likawekwa,” alisema, halafu akakatiza, akaendelea
kulia.
Wenzake
walimtoa nje. Baadaye walieleza waandishi wa habari kuwa Khamis alipata mshtuko
wa moyo, wakampeleka hospitali ya Amana.
Mwenyekiti
wa chama hicho, James Mbatia alisisitiza kuwa Khamis amewathibitishia kwa dhati
kwamba hakuwahi kushiriki katika kuandaa wala kupitisha Katiba inayopendekezwa
tangu BMK liliporejea kwa mara ya pili Agosti 5 mwaka huu.
“Kitendo
cha kuandika jina la kiongozi wetu wa taifa katika katiba hiyo bila ridhaa wala
ushiriki wake ni ulaghai uliokithiri kwa Watanzania na dunia kwa ujumla.
Kitendo hicho ni udhalilishaji kwa ndugu Haji Ambar Khamis yeye binafsi,
familia yake, chama chetu, viongozi na wanachama wote wa UKAWA pamoja
Watanzania kwa ujumla wao,” alisema.
Mbatia
alisema baada ya kupata nakala ya katiba hiyo inayopendekezwa, yeye na wenzake
waligundua kuwa jina la kiongozi wao lilikuwa miongoni mwa wajumbe waliopiga
kura kupitisha katiba hiyo.
Alisema
walipomuuliza kuhusu ushiriki wake kwenye mchakato huo, alikanusha kwa kiapo.
Mbatia
alisema pia kuna ushahidi wa kutosha kwamba muda wote tangu Aprili mwaka huu,
Khamis hakushiriki katika vikao vya BMK.
Kwa
mujibu wa Mbatia, chama chao kinaamini kuwa kitendo hicho kimefanywa kwa
makusudi na viongozi wakuu wa BMK ili kukidhi haja zao binafsi na kulaghai umma
wa Watanzania, na ni ishara hatarishi kwa usalama wa taifa kwani kinaweza
kusababisha machafuko nchini.
Alisema
uongozi wa chama umepokea Katiba inayopendekezwa kwa fedheha na mshtuko mkubwa
na unaamini kuwa kuna mkakati mbaya na wa makusudi wa kusambaratisha chama
chao.
“Imani
hii inatokana na ukweli kwamba tangu mchakato wa kupata katiba umeanza, tayari
tumeshapoteza viongozi wetu wawili kwa namna za kutatanisha, na hakuna majibu
yanayoeleweka kutoka kwa vyombo vya dola,” alisema.
Alisema
miongoni mwa viashiria hivyo ni mauaji ya kikatili na ya kinyama ya aliyekuwa
kiongozi wa chama hicho Dk. Edmund Sengondo Mvungi yaliyotokea Novemba mwaka
jana, na aliyekuwa mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa na Kamishna wa chama
hicho Mkoa wa Mara, Stephen Sebeki yaliyotokea Julai mwaka huu.
Mwenyekiti
huyo aliongeza kuwa, wana hofu kubwa juu ya usalama wa chama ngazi mbalimbali,
wanachama wote wa chama hicho na wanasiasa wenzao wa UKAWA.
Alisema
chama chake kitafanya utafiti wa kina na kuchukua hatua za kisheria.
Wanajadiliana na jopo la wanasheria juu ya suala hilo.
Mbatia
aliitaka serikali iwajibishe wote walioshiriki kubuni na kuandaa mkakati wa
kuchomeka jina la Khamis katika orodha ya wajumbe wa Zanzibar.
Vile
vile, alimtaka Sitta, amuombe radhi kiongozi wao huyo, familia yake, ndugu,
rafiki zake, mashabiki wake, chama hicho, viongozi wenza wa vyama vinavyounda
UKAWA pamoja na Watanzania kwa ujumla kwa hujuma walizomfanyia.
“Kisha
tunaitaka serikali itoe tamko la kuhakikisha usalama wa kutosha kwa kiongozi
wetu, familia yake, viongozi wote wa NCCR pamoja na wanasiasa wote nchini na
familia zao. Pia watuhakikishie kwamba matukio ya mauaji kama yaliyowahi
kuwatokea viongozi wetu hao wawili hayatatokea tena,” alisema.
Bunge
Maalum la Katiba lilimalizika Oktoba 4 mwaka huu, na kuikabidhi katiba hiyo
inayopendekezwa kwa Rais Jakaya Kikwete, Oktoba 8 mwaka huu.
Kumekuwapo
na utata juu ya mfumo aliotumia Sitta kupata theluthi mbili ya wajumbe wa
Zanzibar. Baadhi ya wachambuzi wamesisitiza mara kadhaa kwamba idadi ya wapiga
kura kutoka Zanzibar ilighushiwa.
Utata
ulitokana na kauli za Sitta mwenyewe, kwani awali alisema idadi ya wajumbe wote
wa BMK ni 629 (Tanganyika 419 na Zanzibar 210). Idadi hiyo iliongezeka baadaye
wakati wa kutangaza matokeo, ikawa 219 kwa wajumbe wa Zanzibar.
Theluthi
mbili za wajumbe 210, ni 140. Wajumbe wa kundi linaloojiita Umoja wa Katiba ya
Wananchi (UKAWA), akiwamo Khamis, walikuwa 67. Waliopiga kura za wazi za
“hapana” walikuwa wanane, na kufikisha wajumbe 75. Kwa idadi hiyo tu, wapiga
kura kutoka Zanzibar walibaki 135.
Kwa
idadi ya wajumbe 219, theluthi mbili ingekuwa ni 146, lakini kwa kuzingatia
kura za “hapana” zilizopigwa, idadi inayobaki ni 144. Kuibuka kwa mjumbe mpya
na madai haya, kunaongeza utata juu ya theluthi mbili iliyotangazwa na Sitta
juu ya idadi ya wajumbe waliopitisha katiba hiyo.
Sitta
alipotafutwa ili atoe ufafanuzi, simu yake iliita lakini hakupokea. Baadaye,
mwandishi alimtumia ujumbe mfupi wa maandishi, hakujibu.
Kwa
mujibu wa Kamusi ya Kiswahili Sanifu, neno -fyanda lina maana ya –bana, -finya.
Hiki ni kibano kipya kwa Sitta, ambaye kwa siku kadhaa amekuwa katika mzozo na
viongozi wa dini na wanasiasa wenzake, hasa wa upinzani na makundi kadhaa
katika jamii.
SORCE: TANZANIA DAIMA .
0 comments: